Sunday, March 3, 2013

Kutoka BoT


BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imeruhusu kuwapo shughuli za uwakala utakaotoa fursa kwa mtu au kampuni kuingia mkataba na benki yoyote nchini na kuendesha huduma kama wakala kwa niaba ya benki husika.

Lengo la kuanzisha huduma za uwakala wa benki nchini ni kuwezesha wananchi kupata huduma za kifedha kwa karibu na kirahisi zaidi pamoja na kuweka mfumo sawa wa utoaji huduma hizo katika njia ambayo inatoa unafuu wa gharama kwa watumiaji.

Mkurugenzi wa Huduma za Kibenki wa BoT, Emmanuel Boaz alisema jana kuwa kupitia wakala, benki zitatumia maduka, vituo vya mafuta, shule na taasisi kadhaa kutoa huduma bila kulazimika kujenga majengo ya matawi.

Alisema benki zitaruhusiwa kutoa huduma kupitia wakala baada ya kupata kibali kutoka BoT na kwamba utoaji wa kibali utazingatia utimizaji vigezo vilivyoainishwa katika mwongozo ikiwa ni pamoja na kuwa na mtaji.

 Alitaja vigezo vingine kuwa ni kuthibitisha uwezo kimapato na kuwa na historia nzuri ya kutimiza matakwa ya kisheria, kanuni na maelekezo kuhusu biashara ya benki.

Boaz alisema benki zitakazoruhusiwa kufanya hivyo zitatakiwa kuwa na mkataba unaozingatia mwongozo wa uwakala. Alisema mkataba hautakuwa na kipengele cha kuzuia wakala kuingia mkataba wa uwakala na benki zingine.

Alitaja baadhi ya vigezo vya uwakala kuwa ni mhusika awe amefanya biashara halali kisheria katika muda usiopungua miaka miwili na biashara husika iwe endelevu.

Alisisitiza kuwa biashara ya wakala wa benki haitafanywa na kampuni au mtu yeyote asiye na biashara nyingine ya msingi.

Alisema vigezo vingine ni pamoja na kuwa na leseni ya biashara, kuwa na sehemu ya kudumu ya biashara, kutokuwa na mkopo chefuchefu katika benki; kuwa na wafanyakazi wenye uwezo wa kufanya uwakala.

Alisema wakala atakuwa akipokea na kutoa amana za wateja, kusaidia wateja wenye amana kufanya malipo na ulipaji mikopo. Shughuli zingine ni kusaidia wateja kulipa Ankara na kufanya malipo kwa ajili ya akiba ya uzeeni.

Mawakala pia watasaidia wateja wa benki kutuma fedha ndani na nje ya nchi, maulizo ya salio na kutoa kwa wateja wa benki ripoti fupi ya akaunti zao.

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...