Dar es Salaam. Siyo tetesi tena. Sasa ni rasmi kwamba Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amekuwa akitajwa kuwania urais amethibitisha
wazi kuwa atagombea kiti hicho katika uchaguzi mkuu mwakani.
Alitoa uthibitisho huo juzi akiwa London,
Uingereza ambako yuko katika shughuli za kikazi. Hatua hiyo inaondoa
uvumi ambao umekuwapo kwa takriban miezi mitatu sasa kwamba naye tayari
ameingia katika kinyang’anyiro hicho.
Pinda aliweka wazi nia ya kuelekea Ikulu
akisisitiza kuwa hajatangaza rasmi lakini akasema kuwa ameanza harakati
hizo ‘kimyakimya’. Alikuwa akijibu moja ya maswali aliyoulizwa katika
Kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na Shirika la Utangazaji la
Uingereza (BBC).
Alitamka rasmi kuwania nafasi hiyo baada ya
kuulizwa kuwa anafikiri ni kiongozi gani anayefaa kurithi mikoba
itakayoachwa na Rais Jakaya Kikwete.
“Mikoba ya Rais Kikwete inaweza kuchukuliwa na
yeyote atakayeonekana mwisho wa safari kwa utaratibu wa chama na ndani
ya Serikali .... kama anafaa. Waliojitokeza sasa ni wengi na mimi
ninadhani ni vizuri,” alisema Pinda.
Alipoulizwa kama yupo miongoni mwa wengi alisema,
“… umesikia kama nimo … basi tukubali hilo na yeye Waziri Mkuu yumo. Hao
wote waliojitokeza pamoja na Waziri Mkuu aliyejitokeza ni katika
jitihada za kusema hebu Watanzania nitazameni je, mnaona nafaa au
hapana?”
“……..fanyeni hivyo kwa mwingine na mwingine,
mwisho wa yote zile kura zitakazopatikana kwenye mkutano mkuu kama ni
kutokana na chama kile kinachotawala na hatimaye Watanzania
watakaojitokeza kupiga kura Oktoba kutokana na wagombea watakaojitokeza
kutoka kwenye vyama mbalimbali huyo ndiye tutakayempata kama rais. Hivyo
natangaza nia hiyo kimyakimya.”
Kiongozi huyo atakuwa wa pili kutangaza nia hiyo
kupitia vyombo vya habari vya kimataifa, baada ya Naibu Waziri wa
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
Alitangaza nia hiyo Julai 2, 2014, alipokuwa
Uingereza katika mkutano wa sekta ya mawasiliano baada ya kuhojiwa
kwenye kipindi hicho hicho cha Dira ya Dunia.
Urais CCM
Kuingia kwa Pinda katika mbio za urais kupitia CCM
tayari kumebadili mwelekeo wa kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kubwa ya
uongozi nchini kutokana kuzigawa baadhi ya kambi za wagombea ambao
walikuwa wakitajwa kwa muda mrefu kabla yake.
Wengine ambao wamekuwa wakitajwa kuwania nafasi
hiyo kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri Mkuu
Mstaafu Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu),
Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi na
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
0 comments:
Post a Comment